Friday, May 15, 2015

NAMNA SAHIHI YA KUPUNGUZA KITAMBI NA UNENE




Mtindo wa maisha, vyakula na shughuli za kila siku za mwanadamu ni baadhi ya vitu vinavyosababisha idadi kubwa ya wake kwa waume kuwa na uzito au unene kupita kiasi na wakati mwingine kuwa na vitambi.

Matatizo haya yamekuwa yakiwapata watu wa jinsi zote na kuwanyima raha wanawake wengi, ambao hufikia hatua ya kutumia mikanda maalumu ya kufunga tumbo au kuhangaika kupitia njia mbalimbali ili kupunguza kadhia hiyo kwao.

Kutokana na kuongezeka kwa tatizo hilo, kumezuka dawa nyingi zinazodaiwa kuwa na uwezo wa kupunguza vitambi na uzito mkubwa, lakini wataalamu wa afya wanaonya kuwa ni sumu.

Tafiti nyingi za kisayansi zinaonesha kuwa dawa hizi kwa kiasi kikubwa zina kemikali kama vile phentermine, sibutramine, phenolphthalein, caffein, hydroxycitric acid (HCA) na senna ambazo zina madhara makubwa kwa afya ya mwanadamu.

Dk. Phil McGraw anasema baadhi ya dawa hizo huathiri sehemu ya ubongo inayohusika na hamu ya chakula.  "Hamu ya chakula ni muhimu kwa ajili ya ubora wa afya na maisha.  Dawa yoyote inayoharibu hamu ya chakula kwa kipindi kirefu, inaweza kusababisha madhara ya kiafya", anasema Dk. Phil.

Mama mwenye uzito wa kilo 108, Doreen Shayo anasema amewahi kujaribu dawa za kupunguza mwili, lakini akapatwa na homa kali iliyohatarisha maisha yake baada ya wiki moja, hivyo alishindwa kuendelea na dozi hiyo.

"Nilishawishiwa kununua dawa hiyo ya kupunguza uzito na nilishauriwa kula mbogamboga, matunda na maji kwa wingi wakati wa dozi, sikuwa nakula wanga wala chakula kamili.  Nilipata homa ya ghafla madaktari wakanishauri kwamba dawa zile hazikuwa nzuri kwangu hivyo niachane nazo, wakati huo nilikuwa na kilo 120 lakini nilipungua kutokana na maelekezo ya madaktari", anasema Doreen.

Baadhi ya madaktari bingwa wa afya ya binadamu wanasema msukumo wa dawa hizo unaowafanya wahusika kuharisha mafuta mengi kwa wakati mmoja, ni njia isiyo sahihi ambayo pia huathiri baadhi ya viungo ndani ya tumbo, huku madhara yake yakijitokeza miaka kadhaa mbeleni.

Tabibu wa tiba mbadala kutoka kituo cha Fore Plan Clinic, Juma Mwaka anasema asilimia kubwa ya dawa za kupunguza kitambi na mwili kwa uharaka ni sumu.

"Mtu anapewa dawa anaharisha sana, swali la kujiuliza nini dawa inafanya tumboni na kusababisha kupata choo laini au kuyeyusha mafuta kwa muda mfupi?  Lazima tujue kwamba zina madhara baada ya muda, wengi wanauziwa vitu vibaya na mbegu fulani ambazo ni sumu halafu mwili unabadilika anaharisha sana, anaambiwa dawa ndio inafanya kazi yanatoka mafuta mengi, si njia sahihi ya kupunguza uzito wa mwili au kitambi."

Dk. Samuel Shita kutoka Hospitali ya Mwananyamala anasema kwa kawaida kuharisha humfanya mtu kupunguza maji mengi na chumvichumvi mwilini na hivyo huathiri kazi ya seli na mfumo wa fahamu.

"Dawa hizo nyingi hazijaruhusiwa kutumika na Wizara ya Afya na wala hazijathibitika kwamba ni sahihi kwa matumizi ya binadamu, lakini wanazitumia na madhara yake yanaanza kujitokeza baada ya kutumia mtu anaharisha sana na yeye anadhani ana mafuta lakini ule ni uteute unaokaa tumboni unaosaidia tumbo kufanya kazi.

"Utafiti unaonesha kuwa watu wanaopendelea kula katika migahawa mikubwa ndio wanaoongoza kuwa na miili mikubwa, teknolojia zipo na dawa zitumikazo lazima ziwe zimefanyiwa utafiti kwa zaidi ya miaka 10.  Kuna madhara mengi yanayoweza kuwakuta watu ikiwamo ya figo, moyo, ini na mishipa ya damu."

Dk Shita anasema kuna njia sahihi za kupunguza tumbo ambazo pia ni salama.  "Mtu anatakiwa kufanya mazoezi mepesi na matumizi sahihi ya vyakula, tunatakiwa kupunguza vyakula vya wanga kupita kiasi, sukari na mafuta.  Pia tunatakiwa kupunguza mafuta yatokanayo na wanyama kwa kuwa yana Cholesterol nyingi na ulaji holela."

Anasema soda, pipi na chocolate ni vyakula ambavyo havitakiwi kutumika kupita kiasi.

Mwaka anazitaja hatua sahihi za kupunguza kitambi na kuondoa sumu mwilini akisema: "Kutumia juisi za matango, karoti na nyanya kila siku kwa muda wa mwezi mmoja sumu zote zinaondoka."

Hata hivyo, Mwaka anasema mtu anapokula chakula ni lazima kiishe tumboni kabla ya kuingiza kingine, vinginevyo anakuwa ametunza sumu mwilini kutokana na kuwa na mabaki maengi ya chakula cha takriban hata mwaka mmoja.

"Mfuko wa chakula una uwezo wa kutunza chakula kwa muda mrefu, ndiyo maana binadamu hufa akikosa chakula kwa siku nyingi.  Miongoni mwa vitu vinavyofanya uondoe sumu mwilini ni kufuata sheria za ulaji na njia za asili za kuondoa sumu hiyo na si njia za haraka kwani zina madhara," alisema.

Wataalamu wa masuala ya dawa Deborah Mitchel na David Dadson, katika kitabu chao kilichochapishwa mwaka 2002 cha "The Diet Pill Guide: The Consumer's Book of Over-the-Counter and Prescription Weight -Loss Pills and Supplements," wanasema:

"Ingawa ushahidi wa dawa hizi unazidi kuongezeka, bado watu wengi wanaaminishwa kwa uongo kuwa zina manufaa.  Hata hivyo, pia watu wanaendelea kuamini kuwa dawa hizi zinazotokana na mimea na ni dawa salama za asili zinazofanyiwa utafiti wa kina na kuthibitishwa na mamlaka za udhibiti na usalama wa dawa kama nyingine za hospitalini."

Namna ya kupunguza kitambi


Mwaka anasema maji ya moto yakitumiwa kwa umakini yana uwezo wa kupunguza kitambi, tumbo au uzito mkubwa wa mwili kwa asilimia 60.

"Maji ya moto yana uwezo wa kupunguza tumbo kwa zaidi ya asilimia 60, unachotakiwa kufanya ni kuyachemsha yawe ya vuguvugu kiasi kunywa kati ya glasi nne mpaka sita na iwe ni katikati ya mlo mpaka mlo ndiyo maana kuna watu wanashauri unywe asubuhi au iwe katikati ya mlo wa jana usiku na ule utakaokwenda kuula baadaye.

"Lakini pagumu zaidi ni pale ambako kabla hujakwenda kupiga mswaki ndiyo unatakiwa kuyanywa haya maji.  Tunapata vitamin B12 ambazo zinazalishwa mdomoni wakati binadamu akiwa amelala na mojawapo ya vitamin hiyo ni pamoja na kusaidia msagiko (mmeng'enyo) ule wa vyakula."

Anasema tatizo la wengi kukaa na vyakula kwa muda mrefu tumboni, ni moja ya sababu pia ya kuwa na tumbo kubwa yaani kuwa na mafuta ya ziada tumboni na wengine wanakuwa na vyakula vingi wanavyoingiza kuliko wanavyovitoa.


"Asubuhi kabla hujapiga mswaki ukaondoa zile vitamin mdomoni zinywe pamoja na maji, kunywa maji ya vuguvugu glasi nne mpaka sita kila siku unapoamka asubuhi mfululizo mpaka siku 21, baada ya muda fanya hivyo kwa wakati mwingine na wakati ukifanya hivyo pia epuka vile vitu vitakufanya uendelee kuwa na tumbo ili unachokifanya kiweze kuwa na majibu na si kuoga na kujipaka tope," anasema na kuongeza kuwa kupunguza vyakula vya wanga ni njia mojawapo itakayomfanya mhusika kupata majibu ya haraka.
Share:

6 comments:

  1. Naitwa seif niko tanga ni mnene mpaka sina raha wenzangu wanicheka nifanyeje

    ReplyDelete
    Replies
    1. Ahsante Bwana Seif kwa swali, unatakiwa upunguze kula vyakula vyenye mafuta na vyakula vya wanga. Pia, unatakiwa uwe unafanya mazoezi mara kwa mara.

      Delete
    2. Naomba kufahamu vyakula ambavyo havina wanga. Maana naona kama nimezungukwa na wanga tu mie.. Nini hasa cha kukila walau nipunguze uzito wajameni..

      Delete
  2. MAZOEZI YAPI NI MAZURI KWA KUPUNGUZA KITAMBI?

    ReplyDelete
  3. Ugali na wali je vinaongeza uziti na tumbo?

    ReplyDelete