Monday, September 7, 2015

VYAKULA VINAVYODHIBITI UZITO KUPITA KIASI

Spinachi

Uzito kupita kiasi ni jambo la hatari kiafya kwa kila mtu, lakini zaidi kwa watu wenye umri mkubwa, wagonjwa na wale wanaoishi na Virusi Vya Ukimwi (VVU).

Watu wenye uzito kupita kiasi wako katika hatari ya kupata magonjwa mbalimbali yakiwemo shinikizo kubwa la damu, magonjwa ya moyo, kiharusi, kisukari cha ukubwani, miguu kuuma au kuvunjika mifupa.

Uzito kupita kiasi pia, unaweza kuchangia kupunguza hamu na nguvu za kufanya tendo la ndoa kwa wadau wote wawili, hivyo ndoa inaweza kuwa katika wakati mgumu.

Mara nyingi uzito kupita kiasi unasababishwa na mtu kukosa kufanya mazoezi au kazi za kutoka jasho, kuvuta sigara, kunywa pombe kwa wingi na ulaji usiofaa.

Ulaji usiofaa ni pamoja na kula kwa wingi vyakula vya wanga, sukari na vile vyenye mafuta.  Kula kiasi kidogo vyakula vyenye nyuzi lishe kama vile mboga za majani na matunda ni muhimu.

Zaidi walio katika hatari ya kupata uzito kupita kiasi ni wale wale wanaotumia vyombo vya usafiri kwa muda mwingi, wanaokaa ofisini au dukani kwa muda mwingi, wasiokuwa na taarifa za kutosha kuhusu afya na lishe bora na wenye msongo wa mawazo.  Vilevile kuwa na marafiki wasiojali afya zao ni hatari kubwa zaidi ya kuwa na uzito kupita kiasi.

Ulaji saladi ya spinachi, matunda ya epo na parachichi unaweza  kumsaidia mtu kuwa na uzito unaotakiwa kiafya.

Matunda ya Apple


Kabla mtu hajaanza kula mlo wake wa asubuhi, mchana au usiku anashauriwa aanze na mboga za majani za spinachi au aina nyingine.

Saladi iwe chakula cha hamu.  Ulaji wa namna hii unamuwezesha mtu kula kidogo vyakula vyenye wanga, sukari au mafuta ambavyo vina mchango mkubwa wa kuongeza uzito.

Vyakula vyenye wanga vinavyoliwa sana hapa nchini ni kama vile wali, ugali, mikate, maandazi, vitumbua, chapati, viazi vitamu, viazi mbatata, ndizi na chipsi.

Vyakula vyenye sukari ni pamoja na soda, keki, biskuti na asali.  Vyakula vyenye mafuta mengi ni vile vilivyokaangwa ikiwemo chipsi kuku au mayai.

Mlo wa mboga za majani kama vile spinachi unajaza tumbo na kumfanya mtu ajisikie ameshiba na hivyo kuzuiwa tabia ya kutamani kula vyakula vya wanga au sukari.

Mboga za majani za spinachi, pia, zina kirutubisho kinachoitwa thylakoids, ambacho kinachochea mwili kuzalisha homoni inayopunguza hamu ya mtu kutaka kula, hasa vyakula vyenye sukari.

Kuhusu matunda ya epo, kwa siku mtu akila tunda moja ni jambo zuri.  Matunda ya epo yana maji na nyuzi lishe ambazo zinalifanya tumbo kujisikia limeshiba.  Matunda ya epo pia yana kirutubisho cha pectin, ambacho kinakifanya chakula kilichopo tumboni kusagwa kwa muda mrefu na kumfanya mtu kujisikia ameshiba.

Mtu akila tunda zima la epo, (sio juisi) kabla ya mlo, atajisikia hali ya kushiba na hivyo atakula kidogo chakula cha wanga au sukari.
Kwa upande wa matunda ya parachichi, kula nusu ya tunda hilo kwa siku kunaupa mwili mafuta bora kiafya na nyuzi lishe ambazo zinamfanya mtu ajisikie ameshiba muda mwingi na kutokutamani chakula mara kwa mara.

Unapokula kwa wingi vyakula vya wanga, sukari au mafuta, ndipo mwili unaongezeka uzito kupita kiasi. 
Share:

No comments:

Post a Comment