Monday, February 19, 2018

MBOGAMBOGA ZINALETA AFYA BORA KWA ANAYETUMIA



Sehemu kubwa ya mbogamboga (vegetables) inachukuliwa na maji kwa asilimia 84-96.  Kwa upande wa virutubisho vingine, mbogamboga ni chanzo kizuri cha madini ya Phosphorus na Calcium.  Vilevile ni chanzo kizuri cha Vitamin A na C.

Vitamin C inapatikana zaidi kwenye mbogamboga za majani ambazo zina rangi ya kijani, kama vile mchicha, kisamvu, matembele, majani ya kunde na yale ya maboga na kadhalika.  Kwa upande wa vitamin A inapatikana kwa wingi kwenye karoti.

Zaidi ya hayo, baadhi ya mbogamboga zina protini na kabohaidreti (wanga) kwa mapeyasi, maharage na viazi.

Nyuzi nyuzi za kilishe (dietary fibres) pia zinapatikana kwa wingi hasa katika mbogamboga za majani.

Vitamin C ni kirutubisho kinachopotea kwa haraka wakati wa upikaji wa mbogamboga.  Ili kupunguza tatizo hilo, mbogamboga zipikwe kwa dakika chache, kama tano mpaka kumi.  Kwa utaratibu huu, maji yachemshwe kwanza.  Yaani osha mboga zako vizuri kwa maji safi halafu zitie katika maji yaliyochemka.  Baada ya dakika hizo tano mpaka kumi zitakuwa zimeiva kwa kiasi ambacho hakitapoteza vitamin C kwa wingi.

Sambamba na hatua hiyo, mbogamboga lazima zipikwe kwenye chombo kilichofunikwa ili vitamin zisiondoke na mvuke.  Pia, watu wajilazimishe kunywa ule mchuzi (supu) unaopatikana baada ya kupika hizo mbogamboga.  Hii ni kwa sababu, mchuzi huo una vitamin nyingi inayotoka kwenye mbogamboga.

Vitamin na madini ni muhimu sana mwilini.  Kwa sababu zinasaidia kuupa mwili kinga ya maradhi mbalimbali na madini kama ya chuma, yanahitajika kwa utengenezaji wa damu.  Bila damu hakuna binadamu atakayeweza kuishi.

Nyuzinyuzi za kilishe nazo ni muhimu ili chakula kiweze kusagwa vizuri tumboni.  Pia, zinasaidia kunyonya sumu iliyoko tumboni ambayo inaweza kusababisha ugonjwa wa saratani (kansa).  Nyuzinyuzi hizo zinasaidia mtu kupata choo kikubwa mara kwa mara.  Yaani huondoa tatizo la kutopata choo.

Share:

No comments:

Post a Comment