Tuesday, November 29, 2016

SHAMBULIZI LA MOYO (Heart Attack)

heart attack

Wakati gari likitegemea injini kuendeshwa barabarani, mwili wa binadamu hutegemea moyo na endapo utasimama kwa tatizo lolote basi shughuli zote hukoma.

Magonjwa ya moyo ni miongoni mwa magonjwa yasiyoambukizwa.  Inakadiriwa, mpaka ifikapo mwaka 2020 magonjwa ya kuambukiza na yasiyoambukiza yatakuwa na uwiano sawa.  Asilimia 50 kwa 50 kwa kusababisha vifo duniani.

Magonjwa huwakumba zaidi watu wenye kipato kizuri kutokana na tabia yao ya kutozingatia lishe bora.  Wananchi wa mataifa yaliyoendelea wapo kwenye hatari zaidi ya kupata magonjwa haya.  Licha ya ulaji holela, watu hawa hawafanyi mazoezi kama inavyoshauriwa.  Wanakula zaidi vyakula vya wanga na mafuta, wanakunywa pombe na kuvuta sigara bila kujali athari zake.


Shambulizi la moyo au pigo la moyo kama wengine wanavyoliita ni moja ya magonjwa ambayo yanaweza kumpata mtu yeyote.  Limo miongoni mwa yanayoongoza kwa kusababisha vifo vya wanaume na wanawake duniani.

Kwa kawaida, ugonjwa huu hutokea baada ya sehemu ya nyama ya moyo kuharibika au kufa kutokana na kukosa damu ya kutosha.  Yote yanaweza kusababishwa na kuziba kwa mishipa ya damu inayosambaza damu kwenye moyo kutokana na mafuta mwilini.

Waliohatarini

Watu walio kwenye hatari ya kukumbwa na ugonjwa huu ni pamoja na wenye umri mkubwa wa kuanzia miaka 45 kwa wanaume na 55 kwa wanawake, wavuta sigara na wale wenye mafuta mengi mwilini.

Wengine ni wagonjwa wa kisukari, shinikizo la damu, wenye unene wa kupitiliza au kitambi na wenye matatizo ya figo.  Wanywaji wa pombe kupindukia na wanaotumia dawa za kulevya pia hasa cocaine na methamphetamine.  Wengine ni wenye msongo wa mawazo wa muda mrefu au upungufu wa vitamin B2,B6, B12 na folic acid.

Dalili

Maumivu makali ya ghafla kifuani ambayo husambaa kwenye taya, shingo, bega na mkono wa kushoto ni dalili za awali.  Kupumua kwa shida na kutokwa jasho kwa wingi au kuhisi mapigo ya moyo kwenda haraka.  Kichefuchefu, kutapika na kuchoka haraka pamoja na kupoteza fahamu.  Vichomi hasa vinavyosababishwa na vimelea vya chlamydophila pneumonia.  Tafiti mbalimbali zinalihusisha shambulizi la moyo na msongo wa mawazo.

Matibabu

Shambulio la moyo ni tatizo linalohitaji matibabu ya dharura.  Lisipotibiwa kwa haraka huweza kusababisha kifo ndani ya muda mfupi tangu mgonjwa apatwe na tatizo.  Matibabu ya tatizo hili hujumuisha kumuongezea mgonjwa oksijeni na kupewa vidonge vya Aspirini ndogo vinavyozuia damu kuganda pamoja na kuzibua mirija midogo ya damu katika moyo iliyoziba.

Kujikinga

Zipo njia kadhaa za kujikinga na shambulio la moyo ambazo zinajumuisha kutovuta sigara, kufanya mazoezi ya mara kwa mara na kupunguza unywaji pombe.  Kubadilisha aina ya mlo kwa kupunguza mafuta na chumvi, kutumia mafuta ya samaki zaidi na baadhi ya tafiti zinasema uchangiaji damu hupunguza hatari ya magonjwa ya moyo hasa kwa wanaume.

Madhara

Kifo kinaweza kutokea endapo moyo utashindwa kufanya kazi.  Upo uwezekano wa shambulio la moyo kurudia mara ya pili.

Ili kutambua tatizo hili, mwaka 1979, Shirika la Afya Duniani (WHO) liliweka vigezo vinavyojumuisha maumivu ya kifua kwa Zaidi ya dakika 20.
Share:

No comments:

Post a Comment