Tuesday, November 29, 2016

MSONGO WA MAWAZO KWA WAJAWAZITO HUSABABISHA ULEMAVU KWA MTOTO


Mjamzito mwenye msongo wa mawazo anaweza akapoteza kiumbe chake.  Ndiyo, ujauzito unaweza kuharibika kutokana na mawazo mazito ya mama mwenye nao.

Licha ya ukweli kwamba ni ngumu kuishi pasi na mawazo lakini yakipitiliza ni hatari kwa mustakabali wa mama mjamzito.  Watafiti wa sayansi ya tiba wanalihusisha suala hilo pia na ulemavu wanaozaliwa nao watoto toka kwa aliyekuwa na msongo wa mawazo muda mwingi wa ujauzito wake.

Utafiti ulioongozwa na Dk Dorthe Hansen na matokeo yake kuchapishwa kwenye Jarida la The Lancet Medical ulijikita kuchunguza na kuthibitisha ukweli wa dhana hiyo.


Watafiti hao walitumia taarifa mbalimbali za kitabibu zilizohifadhiwa kipindi cha miaka 12 kati ya mwaka 1980 mpaka mwaka 1992 kutoka masjala ya kitabibu.  Watafiti hao waliweza kuwatambua wajawazito waliokumbwa na changamoto za kimaisha wakati wa ujauzito hata miezi 16 kabla ya kupata ujauzito.

Matatizo makubwa ya kimaisha yaliyochunguzwa ni pamoja na msiba wa ndugu, jamaa au rafiki wa karibu, kulazwa kwa mara ya kwanza baada ya kugundulika na saratani ya aina yeyote na ndugu au jamaa wa karibu kupatwa na mshtuko wa moyo.

Mambo haya yalichunguzwa kwa kigezo kuwa, mjamzito yeyote aliyewahi kukumbana nayo ana hatari ya kupata msongo wa mawazo bila kujali tabia yake, kama hana watu wa kumfariji au uwezo wa kukabiliana na hali hiyo.

Watafiti hao wa magonjwa walibaini kuwa msongo mkali wa mawazo wakati wa ujauzito unaweza kusababisha hitilafu kwenye uumbaji hatimaye mtoto kuzaliwa akiwa mlemavu.

Ripoti yao inazidi kuthibitisha matokeo ya tafiti zilizopita kuwa mama mwenye msongo wa mawazo wakati wa ujauzito kutokana na kuachishwa kazi, kutengana na mwenza wake au kufiwa, au sababu nyingine yoyote ana hatari ya kuzaa mtoto mwenye ulemavu.

Miongoni mwa ulemavu unaoweza kujitokeza kwa mtoto husika ni midomo sungura au matatizo kwenye uti wa mgongo.

Kwenye utafiti wao, jopo hilo lilichunguza maendeleo ya mimba kutoka kwa wajawazito wenye msongo uliotokana na sababu zilizobainishwa na wale ambao hawakukutwa na jambo lolote linaloweza kuwapa msongo.

Wajawazito 3,560 ambao walikumbana na matukio yasababishayo mawazo mazito walihusishwa sambamba na wengine 20,299 ambao maisha yao yaliendelea bila kikwazo chochote kinachoweza kusababisha msongo.

Matokeo ya uchunguzi yalionesha kuwa ulemavu na hitilafu za viungo kwa watoto waliozaliwa ulikuwa mara mbili miongoni mwa kundi la wajawazito ambao hawakuwa na hali hiyo kwa kipindi chote cha ujauzito wao.

Utofauti mwingine ulijitokeza kwa wanawake waliokumbwa na msongo wa mawazo mara nyingi zaidi.  Wale waliowahi kukumbwa na hali hiyo kwenye mimba ya mbili zilizotangulia, mfululizo, walikuwa kwenye hatari kubwa zaidi ya kuzaa watoto wenye ulemavu wa viungo tofauti na wale waliowahi kupatwa na hali hiyo mara moja au wale ambao hawakupata.

Tukio lingine lililoongeza uwezekano wa kuzaliwa mtoto mwenye ulemavu wa viungo mjamzito kufiwa na mtoto wake mkubwa ndani ya miezi mitatu ya mwanzo wa ujauzito alionao.

Hatari ya kuzaa mtoto mlemavu iliongezeka iwapo kifo cha mtoto mkubwa kingetokea bila kutarajiwa kwa mfano kwa ajali au janga jingine lolote pasipo kuugua kwa muda mrefu.

Watafiti wanakwenda mbali zaidi na kueleza kuwa msongo mkali wa mawazo huchangia kuathiri uumbaji wa mtoto aliye tumboni kwa kusisimua uzalishaji wa kichochezi cha cortisone ambacho huongeza kiwango cha sukari kwenye damu na kupunguza oksijeni.
Kuongezeka kwa sukari kwenye damu na kupungua kwa hewa safi inayosambazwa na kumfikia mtoto aliye tumboni husababisha kutokea kwa hitilafu ya uumbaji wa viungo vyake hatimaye ulemavu wa viungo atakapozaliwa.

Msongo wa mawazo, kwa mujibu wa utafiti huo, imebainika kumuongezea mjamzito uwezekano wa kutumia vileo au uvutaji sigara na lishe duni kutokana na kupoteza hamu ya kula, hivyo huongeza madhara kwa kiumbe kilichopo tumboni.

Hata hivyo, Profesa Peter Heper wa Chuo Kikuu cha Queen’s cha Belfast, anasema hakushangazwa na matokeo ya utafiti huo.
“tunafahamu msongo wa mawazo husababisha mabadiliko hasa fiziolojia kwenye mfumo wa mwili wa mjamzito hivyo hakuna kitakachozuia yasimfikie mtoto aliye tumboni kupitia kondo la nyuma na kumwathiri,” anasema.

Matokeo haya yanathibitisha dhana ya muda mrefu kuhusu madhara ya uumbaji wa viungo vya mtoto kwa mjamzito mwenye msongo wa mawazo kwa muda mrefu.

Kutokana na ukweli huo, ipo haja ya namna ya kuwasaidia wajawazito kuondokana na hali hiyo ili waweze kujifungua watoto wenye afya njema na salama.

Hilo lisipofanyika jamii nzima italazimika kutumia rasilimali nyingi kwa ajili ya kuwatunza watoto watakaozaliwa kutimiza mahitaji yao kwa kuanzisha vituo vya kuwalelea au kujenga shule nyingi zaidi kwa ajili yao na kuongeza idadi ya wataalamu kwa ajili yao.

Dk pamela Daniel, mtaalamu wa tiba za watoto anaeleza, ili kufanikisha vita ya kukabiliana na msongo, pamoja na jitihada nyingine, ni vizuri mjamzito awahi kupata huduma za afya kwenye hospitali za uhakika ili apewe ushauri nasaha utakaomsaidia kuokoa afya ya mwanaye mtarajiwa na uhakika wa kujifungua salama.

Anafafanua njia nyingine ya kukabiliana na msongo wa mawazo ni pamoja na kuwa muwazi kwa watu wa karibu ambao kwa namna moja wanaweza kumpa ushauri na kumtuliza kiakili kwa kipindi chote kilichobaki cha ujauzito wake. 
Share:

No comments:

Post a Comment