Monday, February 13, 2017

WAJAWAZITO, WAZAZI WANA HATARI YA DAMU KUGANDA KWENYE MISHIPA

Deep vain thrombosis

Tatizo hili kitabibu hujulikana kama Deep Vein Thrombosis au kwa kifupi, DVT.  Wanawake wako katika hatari ya kupata DVT hasa wanapokuwa wajawazito na wiki ya nne mpaka ya sita baada ya kujifungua.

Inakadiriwa, kwa kila wajawazito 1,000 mmoja anapata tatizo hili ingawa kwa uzoefu wangu bado kwenye jamii ya Kitanzania kuna kesi chache zaidi za DVT zinazoripotiwa.

Takwimu zinaonesha, asilimia 80 ya wajawazito wanapata tatizo hili katika mguu wa kushoto.  Endapo halitagundulika na kutibiwa mapema, madhara hatarishi yanaweza kujitokeza.

Mojawapo ya madhara hayo ni kukwanyuka kwa donge la damu kutoka miguuni na kusafiri katika mzunguko wa damu na kwenda kuziba katika mishipa inayotawanya damu kwenye mapafu ambayo hujulikana kama Pulmonary Embolism (PE).

Tatizo hili linapotokea huwa ni jambo la dharura kwani linaweza kusababisha kifo cha ghafla kwa mjamzito husika hivyo kumpoteza mama na mtoto endapo huduma za kumuokoa mtoto hazitatolewa kwa wakati.

Sababu kubwa inayochangia tatizo hili kwa wajawazito na waliojifungua (wazazi) ni uwapo wa kiasi kikubwa cha kichochezi cha estrogen.

Kichochezi hiki ni moja ya kihatarishi cha kugandisha damu kwa urahisi hasa pembezoni mwa mwili, ikiwemo miguu.

Sababu nyingine ni uwepo wa shinikizo kubwa kutoka kwa nyumba ya uzazi inayoongezeka kadri mimba inavyokua.  Hali hii husababisha utiririkaji wa damu kuwa wa taratibu katika mishipa ya damu hasa iliyopo miguuni.  Mazingira ya namna hii yanachangia kuganda kwa damu kirahisi.

Wakati wa kujifungua, wajawazito hupoteza damu nyingi huku uwezo wa mwili kugandisha damu huwa ni mkubwa ukilinganisha na inavyokuwa wakati mwingine wa kawaida.  Hali hii ni moja ya sababu ya kujitokeza kwa DVT kwa wajawazito wakati wa kujifungua au kipindi kifupi baada ya kujifungua.

Bado wanasayansi hawajui ni kwa nini wakati wa ujauzito kiwango cha protini zinazosaidia damu kuganda kinakuwa juu wakati zile protini zinazosaidia damu kuyeyuka zinakuwa chini.

Vilevile, mabadiliko ya jumla ya damu kipindi cha ujauzito pamoja na matatizo mengine ya damu yanawaweka wajawazito katika hatari ya kupata DVT.

Wajawazito wapo katika hatari ya kupata tatizo hili pamoja na wale ambao familia zao zina historia ya kupata tatizo hilo, wenye umri zaidi ya miaka 35 na wanene au uzito uliokithiri.

Wengine ni wavutaji wa sigara, wenye tishio la kifafa cha mimba au shinikizo la juu la damu.  Pia, wanaopewa mapumziko ya muda mrefu kitandani, wenye magonjwa ya mishipa ya damu, waliojifungua kwa upasuaji, waliopoteza damu nyingi au walioongezewa damu.

Habari nzuri ni kwamba tatizo hili na madhara yake ambayo ni tishio ikiwamo la kuzibwa kwa mishipa ya damu katika mapafu (PE) yanaweza kuzuiwa kutokea na kupatiwa matibabu.
Share:

No comments:

Post a Comment