Monday, December 18, 2017

RUNINGA HUSABABISHA UZITO KWA WATOTO


Elimu haina mwisho hivyo ndivyo unavyoweza ukasema baada ya kufanyika kwa utafiti ambao umebaini kwamba runinga ina uwezo wa kumsababishia mtoto kuwa na uzito wa mwili.

Wengi tunaamini kwamba mtoto akiwa mzito ni kutokana na ulaji wa chakula, ila inabainishwa katika utafiti uliofanywa na wanasayansi mjini London nchini Uingereza kwamba runinga ni moja wapo ya sababu ya kumuongezea uzito mtoto akiwa chumbani.

Wazazi hufanya kila jitihada kuonesha mapenzi ya dhati kwa watoto wao ili kuwaridhisha kwa wale wenye uwezo wamejitahidi kuwawekea runinga kwenye vyumba vyao ili watulie majumbani mwao.

Mtoto anapokuwa na runinga katika chumba chake anakuwa huru zaidi kuangalia kwa muda anaoutaka na huenda wengine wanakosa muda wa kula na hata kulala kwa wakati.

Pamoja na mapenzi hayo kwa watoto wazazi watambue kuwa watoto wenye runinga katika vyumba vyao wana uwezekano mkubwa wa kuwa na uzito wa kupindukia kuliko wale ambao hawana hii ni kwa mujibu wa utafiti uliofanywa na wanasayansi.

Utafiti huo uliofanywa na wanasayansi hao umebaini kuwa runinga humsababishia mtoto kuwa na uzito kupindukia.

Watafiti hao kutoka chuo cha wanasayansi walibaini kuwa watoto wa kike ndio wanaoathirika zaidi kwa kuangalia runinga kwa muda mrefu hivyo wanakuwa na uwezekano mkubwa wa uzito wa miili yao kuongezeka.

Watafiti wanasema kuna kila sababu ya kuchunguza uwezekano huo kwa watumiaji wa vipakatanishi (laptops) na simu za mkononi (mobiles).  Wanasema mbali na uzito kupindukia wakati watoto wanapotumia muda mrefu kutazama runinga hupata madhara mengi ya kiafya.

Hata hivyo, watafiti hao wanasema hawawezi kuwa na uhakika kuhusu nini kinachosababisha uhusiano baina ya kutazama runinga na kuongezeka kwa mwili, lakini wanasema huenda sababu ikawa ni watoto wenye runinga vyumbani kusinzia kwa muda mfupi wakitumia muda kuitazama.

Utafiti huo uliochapishwa katika jarida la Kimataifa la International Journal of Obesity ulitathmini data kutoka kwa watoto wadogo zaidi ya 12,000 nchini Uingereza.

Wanasayansi hao walibaini kuwa zaidi ya nusu ya watoto waliokuwa na runinga katika vyumba vyao vya kulala wakiwa kwenye umri wa miaka saba.

Baadae watoto walipofikia umri wa miaka 11, watafiti walipima viwango vya uzito wao wa mwili kulingana na kimo chao cha urefu kwa kuangalia asilimia ya mafuta ya mwili waliyonayo.

Wasichana waliokuwa na runinga ndani ya vyumba vyao wakiwa na umri wa miaka saba walibainika kuwa asilimia 30 ya uwezekano wa kuwa na uzito wa mwili wa kupindukia wanapofikia umri wa miaka 11, wakilinganishwa na watoto wenzao ambao hawakuwa na runinga vyumbani mwao huku wavulana wakiwa asilimia 20.

Mtafiti Dk Ania Heilmann, amesema utafiti unaonesha kuwa kuna ushahidi wa wazi wa uhusiano baina ya kuwa na runinga chumbani kwa mtoto na kuongezeka kwa uzito wa mwili wa mtoto.

Wataalamu nchini

Dk Fazeel Sajeed kutoka hospitali ya Sanitas anasema anaunga mkono utafiti huo kwa kusema mtoto anapotazama runinga mara nyingi anakuwa katika mazingira ya kula.

Anasema mtoto ambaye anaangalia runinga huku anakula huwa anakula chakula kingi ukilinganisha na yule ambaye anakula bila kuangalia runinga.

Anasema hii ni kutokana na akili ya yule mtoto kuwa katika runinga muda wote mtu ambaye anakula bila kutizama runinga ni tofauti na yule ambaye anaangalia na akili yake haifikirii kwenye chakula.

“Nakubaliana na utafiti huu kwani mtoto anapokuwa karibu na runinga anakuwa na uzito mara nyingi watoto hupenda kuangalia huku wanakula na unakuta vyakula wanavyokula ni vile vyenye sukari na mafuta, mfano viazi (chipsi)” anasema

Dk Sajeed anashauri wazazi wawapunguzie watoto muda wa kuangalia runinga sio muda wote mtoto anakuwa kwenye runinga hasa kwa wale ambao zipo vyumbani mwao.

Anaongeza kuwa si vibaya mtoto kutazama runinga ila anatakiwa kutazama vitu ambavyo atajifunza kama mtoto na sio kuangalia kwa masaa mengi hali ambayo itamletea madhara kiafya.

“Kama chumbani kwa mtoto kuna runinga basi ni jukumu la mzazi kuhakikisha kwamba mtoto anapangiwa muda wa kuangalia na mzazi anajukumu la kuhakikisha mtoto haathiriwi na ile runinga aliyomuwekea chumbani”

Anasema mzazi kuwa makini na mtoto pia itaepusha tabia za kuangalia tv bila kuwa na muda wa kutosha kupumzika au kuvifanyisha viungo mazoezi kuliko kukaa sehemu moja kwa muda mrefu hali inayosababisha uzito wa mwili kuwa mkubwa kuliko umri alionao.

Kwa upande wake dokta Katoto Nestory kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) anasema huenda kweli mtoto kuwa na runinga chumbani kwake itamsababishia uzito kwa sababu mtoto anakuwa amekaa sehemu moja kwa muda mrefu

“Ifahamike kuwa uzito wa mwili hupungua kwa kufanya mazoezi kwa hiyo kama mtoto anachukua muda mwingi kukaa akitazama runinga ina maana mwili unakuwa umetulia hivyo kusababisha uzito kuongezeka”

Dk John Vicent anasema suala la mtoto kuwa na uzito kupindukia halina uhusiano wa moja kwa moja na mtoto kuangalia runinga kwa muda mrefu lakini huenda likachangia.

Anasema mara nyingi watoto wanapokuwa likizo au siku ambazo hawajaenda shule hutumia muda mwingi kuangalia tv ikiwamo katuni kwa hiyo anaweza kutumia hata zaidi ya saa moja.

Anadai kwamba mtoto anapokaa kwa muda mrefu sehemu moja anajijengea tabia ya uvivu hii inafanya hata chakula anachokula kutomeng’enywa vizuri na hatimaye mtoto anakuwa na uzito mkubwa na hata kunenepa zaidi.

Dk Vicent anaongeza kuwa tatizo la kuwa na uzito mkubwa si kwa watoto pekee bali hata kwa watu wazima ambao wanakaa sehemu moja kwa muda mrefu.

Nashauri wazazi wawe makini na watoto wao suala la afya kwa mtoto linahitaji umakini wa hali ya juu watambue kuwa mtoto anapokuwa na tv ndani ya chumba chake sio tu kuongezeka kwa uzito kama utafiti unavyoeleza bali inaweza kuvunja maadili ya mtoto.

Wazazi wazungumza

Mkazi wa Temeke Jijini Dar Es Salaam Maimuna Shabani amesema mzazi kumuwekea mtoto tv katika chumba cha kulala sio tu itamsababishia madhara kama hayo ya kuwa na uzito wa kupindukia lakini pia hata maadili hayatakuwepo.

Anasema ni vyema wazazi wakatumia utafiti huu kujifunza na kutambua kwamba runinga chumbani kwa mtoto si jambo jema.
“wanasayansi wamefanya kazi yao kwa kutafiti juu ya madhara yatokanayo na mtoto kuangalia tv kwa muda mrefu awapo chumbani kwake sasa ni jukumu la mzazi kuwa makini”


Maimuna mama wa watoto watatu anaongeza kuwa yeye watoto wake huangalia runinga kwa muda mfupi.  
Share:

No comments:

Post a Comment