Tuesday, January 9, 2018

SIO KILA UVIMBE KWENYE MFUKO WA UZAZI NI SARATANI


Moja ya dalili za saratani za aina nyingi huambatana na uwepo wa uvimbe wa aina mbalimbali kwenye sehemu husika ya mwili kulingana na aina ya saratani.

Dhana hii imezua hofu kubwa kwa miongoni mwa wanawake wengi hasa inapotokea vipimo vikagundulika wana uvimbe ulioota kwenye mifuko yao ya uzazi.

Habari njema ni kwamba, uvimbe huo hautokani na ugonjwa wa saratani, bali husababishwa na sababu nyinginezo kama nitakavyoeleza, ila kwa kuwa hautokani na saratani, sio vyema kufumbia macho kwa sababu zina madhara mengine kwenye mfumo wa uzazi na afya.

Uvimbe huo huitwa uterine fibroids kwa kitaalam, ni uvimbe usiotokana na saratani na mara zote huwa unaota na kukua kwenye ukuta au tabaka lililopo kwenye mfuko wa uzazi.

Uvimbe huu hutofautiana kwa ukubwa wa maumbile na wakati mwingine ukicheleweshwa unaweza kufikia hata ukubwa wa tikiti maji.

Pia, hutofautiana kwa idadi kati ya mwanamke mmoja na mwingine, mwanamke mmoja anaweza akaotwa na uvimbe zaidi ya mmoja kwenye mfuko wake wa uzazi, lakini mwanamke mwingine anaweza akaotwa na uvimbe mmoja tu kwenye mfuko wake na mara nyingi moja ya madhara yanayosababishwa na uvimbe huo ni mkandamizo wa mfuko wa uzazi, huulazimisha kupanuka hadi kugusa kwenye viwambo vya mbavu na hapo ndipo matatizo mengi hujitokeza.

Hata hivyo, wanawake wengi hupatwa na tatizo hilo kwenye mifuko yao ya uzazi, lakini wengi wao hawatambui kama wanalo kwa sababu hauoneshi dalili hadi unapokuwa mkubwa kupita kiasi na kuanza kuleta matatizo kiafya.

Nawashauri wanawake ni vyema wakajenga utamaduni wa kupata vipimo mara kwa mara ili kubaini ukiwa katika hatua za awali na kwa kufanya hivyo, watajiepusha na madhara makubwa ya kiafya yasababishwayo na uvimbe huo.

Kama nilivyoeleza hapo juu, uvimbe huchukua muda hadi kuonesha dalili zake, kama mwanamke mwenyewe hana utamaduni wa kupata vipimo mara kwa mara; au kama utakuwa umedumu kwa muda mrefu, anaweza kuziona dalili kama vile za hedhi iliyopitiliza ambayo baadaye inaweza kumsababishia kupata anemia, maumivu ya mgongo na kiuno.  Pia anaweza kupata haja kubwa kwa shida, maumivu makali chini ya kitovu na hasa ikitokea uvimbe umeshakuwa mkubwa, kupata haja ndogo mara kwa mara kuliko kawaida na kupata maumivu makali wakati wa tendo la ndoa.

Ukiona dalili hizi, ni Dhahiri una tatizo hilo na ni vyema kwenda hospitali kwa ajili ya vipimo na mpango wa matibabu.  Uvimbe unaoota kwenye mfuko wa uzazi japo hauwezi kusababisha saratani, lakini una madhara mengine makubwa kiafya ambayo ni pamoja na matatizo wakati wa kujifungua yanayoweza kuhatarisha maisha ya mama na mtoto hasa kama atakuwa alishika ujauzito akiwa tayari ana uvimbe.  Lakini pia uvimbe huweza kusababisha mwanamke kukosa uwezo wa kushika mimba, mimba kutungwa nje ya uzazi na tatizo lingine kubwa ni mimba kuharibika mara kwa mara.  Sababu kubwa zinazochangia tatizo hili ni matatizo yanayojitokeza kwenye mfumo wa homoni.

Kisayansi, kwenye mwili wa mwanamke kuna homoni (vichocheo) za estrogen na progesterone, huwa zinafanya kazi ya kuchochea maendeleo ya ukuaji wa sehemu ya ndani ya mfuko wa uzazi kwenye kila mzunguko wa hedhi wa kila mwezi.
Share:

No comments:

Post a Comment