Friday, January 5, 2018

UNAWEZA KUPONA KISUKARI UKIBADILI MFUMO WA MAISHA


Takwimu za Shirikisho la Kisukari Duniani (IDF) zinaonesha mtu mmoja kati ya kila 11, ana kisukari.  Kuna zaidi ya watu wazima milioni 425 duniani kote wenye maradhi haya yasiyoambukiza.

Takwimu hizo pia, kwa mujibu wa ripoti ya mwaka jana, zinabainisha kwamba mmoja kati ya wagonjwa wawili wa kisukari hafahamu kama anaugua maradhi hayo.  Hii ni sawa na nusu ya wagonjwa wote milioni 425 ambao ni takriban milioni 212.

Hata wajawazito nao hawako salama.  Ripoti hiyo inaeleza, ugonjwa huo huathiri mjamzito mmoja kati ya sita duniani kote ambako kuna zaidi ya watoto milioni wenye kisukari aina ya kwanza.

Miongoni mwa watu wote wenye kisukari, ripoti inaonesha theruthi mbili ya wagonjwa hao, sawa na milioni 279 wanaishi mjini ambako vyakula vya asili ama ni adimu au ghali zaidi hivyo kuongeza uwezekano wa kupata maambukizi hayo.

Pamoja na ukweli huo, takwimu hizo zinaonesha wagonjwa watatu katika kila wanne wanaishi kwenye nchi maskini au zenye kipato cha kati.  Wawili kati ya watatu au theluthi mbili ya wagonjwa hao ambao ni sawa na milioni 327 wana umri wa kufanyakazi wakiwa na umri kati ya miaka 20 mpaka 64.

Kutokana na ukweli huo, serikali zinatumia gharama kubwa kukabiliana na maradhi hayo.  Inaelezwa, asilimia 12 ya bajeti yote ya afya huelekezwa kukabiliana na kisukari. Mkuu wa Kitengo cha Kliniki ya Kisukari katika Hospitali ya M.P Shah ya jijini Nairobi, Dk Sairabanu Sokwalla anasema wagonjwa wengi bado hawajajigundua kutokana na kutokuwa na utamaduni wa kupima afya zao.

“Asilimia 80 ya wagonjwa wote wa kisukari ulimwenguni wanaishi katika nchi zinazoendelea.  Takwimu zinaonesha hali ilivyo huko Asia, Amerika na Ulaya kutokana na wananchi wake kuwa na utaratibu wa kupima.  Barani Afrika, wengi hawajui kuhusu afya zao,” anasema.

Ukweli kuhusu hilo, unathibitishwa na Winnie Ngiyo, mwanamke wa miaka 32 anayekiri: “Niliharibiwa ujauzito wangu wa pili.  Hapo ndipo nilihitaji uchunguzi ili kujua sababu, majibu yalibainisha kiwango kikubwa cha sukari mwilini mwangu.”

Mkenya huyo anayeishi Mtaa wa Westlands, jijini Nairobi amefunguka na kuweka wazi kisa hicho na namna alivyoweza kupambana na kisukari mwilini mwake, kutoka 23mmol/1 mpaka kiwango cha kawaida, 6.2mmol/1.

Apona kisukari

Baada ya kugundulika miezi 18 iliyopita, jukumu kubwa kwake lilikuwa ni namna ya kuepukana na kisukari kwa kuwa ipo historia katika familia yake, aliyojua ni ugonjwa wa kurithi.

Uzito wake kwa wakati huo ulikuwa kilogram 110: “Nimepunguza kilogram 21, haikuwa rahisi nilianza kunywa maji mengi, kula vyakula kwa kufuata mpangilio wa lishe hata kwa mume na mtoto wangu wa kiume mwenye miaka 10 pamoja na kufanya zaidi mazoezi.”

Hata hivyo Winnie anasema ni rahisi kuishi na kisukari ikiwa utazingatia matibabu na kuacha matumizi ya vyakula visivyofaa kwa mfano unywaji pombe uliokithiri na kutofanya mazoezi.

Yeye anafanya mazoezi mara tatu kwa wiki akitumia saa moja kuushughulisha mwili wake ili kupunguza mafuta.  Kwa kuwa anaamini ulaji wa baadhi ya vyakula ikiwemo pipi, keki au chipsi kwa wingi huongeza tatizo, huviepuka.

“Inapaswa kuzingatia ulaji unaofaa, katika kila mlo nazingatia robo tangu kunakuwa na mbogamboga, matunda na wanga kwa kiasi kidogo sana, zaidi naepuka vyakula vyenye mafuta,” anasema.

Kupunguza madhara ya hayo, anashauri watu wawe na tabia ya kupima afya mara kwa mara kujua kama wana kisukari au la pamoja na kufuatilia matibabu kwa wenye maradhi hayo ili kuchukua hatua za kuudhibiti mapema. “Tabibu wangu aliniweka wazi kwamba nifuatilie matibabu inavyopaswa nitapona.  Hivi sasa sukari yangu imeshuka na ni ya kawaida.  Sasa nimeacha kutumia dawa nimepona,” anasema.

Winnie mwenye mtoto mmoja, ana kiu ya kuwa na watoto watano hata hivyo anasema hajakata tamaa kwani madaktari wamemruhusu kuendelea kuzaa hivyo kuwa na uhakika wa kuongeza waliobaki.

Baada ya kugundulika kuwa na maradhi hayo, familia yake ilimuunga mkono kupambana na maradhi hayo.  Anasema mumewe alihakikisha anakula vizuri na kufanya vitu vinavyotakiwa.

“Tulipopoteza mtoto ilituuma sote hivyo tuliamua kubadili mtindo wa maisha.  Tunaishi maisha mapya, nilikuwa na safari ndefu kupata,” anasema Winnie.  Ili kuhamasisha matibabu ya kisukari, Winnie ameunda kundi la mtandao wa Whatsapp analolitumia kutoa elimu kwa wagonjwa walio katika matibabu namna ya kukabiliana na ugonjwa huo.

Dk Sokwalla anasema ugonjwa wa kisukari husababishwa na mtindo wa maisha na mara nyingi waathirika wakubwa ni wanawake.  Anazitaja sababu kuu za kisukari kuwa ni uzito kupita kiasi na kutozingatia lishe na ulaji unaofaa huku akitahadharisha kukua kwa maradhi hayo kitakwimu.

Tanzania

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu anasema kwa bahati mbaya, watu wengi hawajitambui kuwa na ugonjwa huu na wengine wanakuwa na dalili lakini hawachukui hatua mapema.

Alisema katika nchi kumi zinazoongoza kwa kisukari barani Afrika, Tanzania inashika nafasi ya nne na hadi mwanzoni mwa mwaka jana, Zaidi ya watoto 2,000 wameingizwa kwenye rejista za watoto kwenye kliniki.

“Asilimia 80 ya wagonjwa wote wa kisukari wapo kwenye nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania.  Utafiti wa mwaka 2012 uliohusisha wilaya 50 nchini ulionesha asilimia 9.1 ya Watanzania wenye umri wa miaka 25 na kuendelea wana ugonjwa wa kisukari,” alisema Ummy.
Share:

No comments:

Post a Comment