Friday, February 9, 2018

NAMNA YA KUTIBU MIMBA CHANGA ILIYOTOKA



Aina ya utokaji mimba itakayoelezwa ni ile ijulikanayo kama utokaji mimba usio kamili ‘incomplete abortion.’

Yawezekana mjamzito alikuwa ana tatizo la mimba kutishia kutoka lakini baadaye hali hiyo inaweza kubadilika na mimba hiyo kutokana na kuharibika, ikabakisha mabaki yaliyoharibika kwenye nyumba ya uzazi.

Hali hiyo inapojitokeza ina maana ujauzito huo umeharibika, hakuna uhai wa mimba hiyo lakini mwili nao umeshindwa kutoa mabaki yote ya kiumbe kilichopo katika nyumba ya uzazi.

Utokaji mimba usio kamili mara nyingi hutokea katika muhula wa kwanza wa ujauzito.  Sababu za utokaji mimba wa aina hiyo ni sawa na aina zingine za utokaji wa mimba changa ikiwamo ile inayotishia kutoka.

Utokaji mimba usio kamili huambatana na utokaji wa damu kwa wingi ukeni ambao si wa kawaida ukilinganisha na utokaji wa damu ya hedhi.

Mgonjwa hutokwa na damu mfululizo ikiwa na mchanganyiko wa mapande ya tishu yaliyochanganyika na damu huku ikiambatana na maumivu makali yasiyovumilika wala kupotea katika eneo la chini ya kitovu na kusambaa kiunoni.

Tabibu au daktari anayekuhudumia pale atakapochunguza atagundua mlango wa nyumba ya uzazi umefunguka huku mabaki ya kiumbe mengine yakiwa yamebaki ndani ya nyumba ya uzazi.

Wakati mwingine hali hii inapotokea inaweza kuambatana na homa, kuhisi kishiwa nguvu, kuonesha dalili za hofu au kuchanganyikiwa.

Hivyo ni vizuri pale unapoona dalili hizi, chukua hatua ya haraka kufika hospitali upate matibabu.

Matibabu yake huwa ni rahisi na ni jambo linaloruhusiwa kisheria, pale inapobainika mimba imeharibika na kutoka yote, mgonjwa atalazimika kusafishwa kwa kuzingatia maadili ya kitabibu.

Usafishaji huu una lengo la kuondoa mabaki yote yaliyopo ndani ya nyumba ya uzazi.

Uwapo wa mabaki katika nyumba ya uzazi unaweza kuzidi kusababisha damu kutoka kwa wingi na pia kuwa makaribisho ya maambukizi ya bakteria.

Mgonjwa atatakiwa amsimulie historia nzima kwa daktari ili abaini chanzo ili kusudi tatizo hilo lisijitokeze katika mimba zingine hapo baadaye.

Uchunguzi unaweza kufanyika ili kujua kama chanzo ni maambukizi ikiwamo kaswende na virusi mbalimbali vinavyochangia mimba kutoka.

Dawa za kudhibiti maumivu na dawa za antibiotiki hutolewa ili kukukinga na maambukizi ya bakteria baada ya kusafishwa.

Ni muhimu kwa mgonjwa wa tatizo hili kufikishwa katika huduma za afya zinazotambulika ikiwamo vituo vya afya vya Serikali.

Ikumbukwe kuwa matibabu ya vichochoroni yanafanyika kwa kutozingatia kanuni za kitabibu, hivyo mgonjwa anakuwa katika hatari ya kusafishwa na vifaa vyenye maambukizi ya vimelea mbalimbali ikiwamo virusi vya ukimwi.  

Share:

No comments:

Post a Comment