Tuesday, February 13, 2018

TATIZO LA MUWASHO NDANI YA KOO



Muwasho ndani ya koo unatokana na sababu mbalimbali japo kwa kiasi kikubwa unachangiwa na mzio (aleji) wa vitu ikiwamo ile itokanayo na baadhi ya vyakula.

Kupitia mzio unaotokana na vyakula, hutokea pia wakati kinga ya mwili inapambana na vimelea vilivyopo kwenye vyakula tunavyokula vyenye kuhatarisha afya zetu.

Kwa kawaida, kinga ya mwili hupambana na vimelea hivi vya maradhi muda mfupi baada ya kula vyakula vyenye vimelea vya maradhi.

Lakini kwa watu wengine, mzio unaweza kutokea hata siku kadhaa baada ya kula vyakula hivyo.

Mzio unaweza kuwa wa kawaida ukiambatana na dalili chache zikiwamo za muwasho ndani ya koo au mdomoni.

Hata hivyo, mara chache inaweza kutokea kuleta madhara makubwa zaidi kiafya.  Hivyo ni vyema kuwa makini katika ulaji wa baadhi ya vyakula kama ngano, baadhi ya aina za kunde, baadhi ya nyama mbichi, mayai na hata maziwa.

Vyote hivyo mara nyingi husababisha mzio kwa walio wengi.
Mzio hutokea pia kutokana na matumizi ya aina mbalimbali za dawa ambazo husababisha muwasho ndani ya koo.

Wengi wanaoshambuliwa na mzio unaotokana na matumizi ya dawa hasa kiantibayotiki kama vile penicillin zinazotumika kuzuia maambukizi ya vimelea mbalimbali.

Mzio huu unapotokea huleta ishara mbalimbali mwilini ikiwamo muwasho ndani ya koo.

Mtu anapokuwa na mafua makali hasa wakati wa baridi, maumivu na muwasho ndani ya koo yanaweza kuongezeka mara dufu vikiambatana na hali ya homa na maumivu ya kifua.

Muwasho huu unaweza kudumu kwa muda usipopatiwa tiba na unaweza kuwa hatari kwa afya.

Muwasho ndani ya koo pia unasababishwa sana na maambukizi ya kibakteria na yale yatokanayo na baadhi ya virusi vya maradhi mbalimbali.

Kuna maambukizi ya maradhi ambayo mara nyingi hutokea kooni ambayo kwa kitaalamu yanaitwa “streptococall” au “strep throat”.
Maambukizi haya yanapotokea yanaweza yakaambatana na vidonda kwenye koo ambavyo wengi pia huwa wanavipata (tonsillitis) yakiambatana na muwasho ndani ya koo hatimaye kuongezeka na kuleta maumivu makali kwenye koo.  Baadhi ya virusi vinavyosababisha mafua pia vinaweza kuleta muwasho ndani ya koo.

Ni Dhahiri kuwa, kila mmoja anafahamu umuhimu wa maji kwenye maisha yetu ya kila siku na hasa kwa afya.

Ukosefu wa kiwango cha kutosha cha maji unasababisha kwa kiasi kikubwa sana tatizo la muwasho ndani ya koo.  Upungufu wa maji mwilini unatokea pale ambapo mwili unapoteza kiasi kikubwa cha maji kuliko kile kinachoingia na mara nyingi hali hii hutokea wakati wa joto sana, baada ya kufanya mazoezi ya mwili au hata wakati wa homa.  Upungufu wa maji mwilini unatokea pale ambapo mwili unapoteza kiasi kikubwa cha maji kuliko kile kinachoingia na mara nyingi hali hii hutokea wakati wa joto sana, baada ya kufanya mazoezi ya mwili au hata wakati wa homa.  Upungufu wa maji mwilini unaweza kusababisha kukauka kwa mdomo, japo hali hii huwa ni ya muda kwa sababu mdomo na koo havipati mate ya kutosha kutokana na upungufu wa maji mwilini na hivyo kupelekea kupata muwasho ndani ya koo.

Utendajikazi wa madawa mwilini pia unasababisha muwasho ndani ya koo.

Baadhi ya madawa yanaweza kusababisha kikohozi kikavu na muwasho ndani ya koo ambayo hayatokani na aleji zinazotokana na dawa.  Watu wanaotumia baadhi ya dawa za shinikizo la damu wanapaswa kutambua kuwa dawa hizo zinaweza kusababisha kikohozi kikavu na muwasho ndani ya koo wakati wa utendaji kazi wake mwilini.  Kwa kawaida dalili hutokea mara tu baada ya kutumia dawa hizi na mara zote haziambatani na dalili zingine tofauti na muwasho ndani ya koo na kikohozi kikavu.

Kwa kawaida huwa si rahisi kugundua kama muwasho ndani ya koo umetokana na baadhi ya magonjwa au ile inayotokana na baadhi ya vyakula, hivyo ni vyema kuzitambua dalili zake ndipo utagundua kama muwasho huo umetokana na vyakula au maradhi mengine.

Share:

No comments:

Post a Comment