Monday, June 29, 2015

MAZOEZI YA MIFUPA

borne exercise
Kama ilivyo misuli ya mwili, mifupa nayo ni tishu zenye uhai zinazofaidika kwa mazoezi ya mwili. Mazoezi huimarisha mifupa na kuifanya iwe na nguvu, iwe na umbo zuri pamoja na ujazo mzuri.
Kwa kawaida mifupa huendelea kukua na kuwa imara katika miaka ya utotoni hadi wakati wa ujana kabla ya miaka 30. Baada ya kipindi hiki cha umri, mifupa taratibu inaanza kupoteza uimara wake na katika kipindi hiki ndipo mazoezi yanapohitajika zaidi. Mazoezi yanasaidia kuimarisha misuli inayojishikiza katika mifupa na kuwa na stamina, mambo ambayo yanapunguza uwezekano wa mtu kuanguka ovyo na kuvunjika mifupa.
Mazoezi yanayoimarisha afya ya mifupa ni muhimu hasa kwa wagonjwa wenye udhaifu wa mifupa, watu wanaofanya kazi za kukaa ofisini muda mrefu, wazee na wanawake waliokoma kupata siku zao za hedhi.
Mazoezi mazuri kwa ajili ya uimara na afya ya mifupa ni yale yanayohusu na mwili kubeba uzito.
Mifano ya mazoezi haya ni kama vile kubeba vitu vizito, kupiga pushapu, kupanda milima, kupanda ngazi, kukimbia taratibu, kutembea kwa muda mrefu pamoja na kucheza muziki unaohitaji minenguo ya aina mbalimbali.
Mazoezi haya pia, yanaweza kuchanganywa na mazoezi ya kuimarisha afya ya moyo na misuli. Mazoezi kama vile kuogelea, kuruka kamba na kuendesha baiskeli yanaweza pia kusaidia moyo na misuli kuwa na nguvu.
Kabla ya kuanza mazoezi yanayoimarisha mifupa, ni jambo la busara kupata ushauri wa kitabibu. Jambo hili ni muhimu hasa kwa watu wenye magonjwa ya muda mrefu kama vile udhaifu wa mifupa, maumivu ya mgongo, kisukari, matatizo ya moyo na figo, shinikizo la damu, kifafa na unene wa kupindukia.
Watu wazima wenye miaka zaidi ya 40 ambao kwa kawaida hawana mazoea ya kufanya, nao wanatakiwa kupata ushauri wa kitabibu kabla ya kuanza mazoezi ya kuimarisha mifupa yao. Mazoezi ya kuimarisha mifupa sharti yafanyike kila siku au mara tatu katika kipindi cha juma moja na yasiwe chini ya dakika 30 kwa siku.
Shirika la Afya Duniani (WHO) katika chapisho lao la mwaka 2010 linalozungumzia umuhimu wa mazoezi kwa afya (GRPAH), linapendekeza watu wenye umri kuanzia miaka 18 na kuendelea, wafanye mazoezi mepesi angalau kwa dakika 150 au mazoezi mazito angalau kwa dakika 75 ndani ya juma moja. Ni vizuri kusikiliza kengele ya mwili wako hasa pale unapoanza mazoezi haya.
Pale unapoanza mazoezi unaweza kuhisi maumivu ya misuli, hivyo basi usijilazimishe kuendelea. Simamisha mara moja mazoezi yako hasa pale unapohisi maumivu ya kifua wakati wa mazoezi na wasiliana na daktari.
Kwa watu wanajali afya ya mifupa yao, pamoja na mazoezi, ni jambo la busara kujiepusha na matumizi ya tumbaku, ulevi wa pombe na matumizi ya dawa za kulevya.
Inashauriwa pia kupata mlo kamili hasa wenye kiasi cha kutosha cha madini ya kalisi (calcium) na vitamini mbalimbali. Dagaa na samaki tunaoweza kuwatafuna na mifupa yao, korosho pamoja na kunywa maziwa kwa kiasi, ni njia bora za kutupatia madini ya kalisi.


Share:

No comments:

Post a Comment